Friday, April 13, 2012

Jeshi lapindua Serikali Guinea Bissau

Friday, 13 April 2012 20:57
VIKOSI vya askari nchini Guinea Bissau vimefanya mapinduzi ya Serikali nchini humo jana, kwa kuzingira makazi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo, makao makuu ya chama tawala na kushikilia redio na televisheni za Serikali.

Vikosi hivyo vimefanya mapinduzi hayo huku nchi hiyo ikitarajiwa kufanya uchaguzi wa marudio Aprili 29, baada ya awamu ya kwanza ya uchaguzi wa Machi 18 kushindwa kutoa mshindi wa jumla wa kura za urais.

Askari hao walivamia makazi ya Waziri Mkuu anayemaliza muda wake, Carlos Gomes Junior ambaye anaongoza katika awamu ya kwanza ya uchaguzi wa rais, huku mwenyewe akiwa hajulikani aliko.

Katika uchaguzi huo wa Machi 18, Gomes ambaye alikuwa akiwania nafasi hiyo kwa tiketi ya chama tawala alishinda kwa asilimia 48.9 na mpinzani wake mkuu, Kumba Yala akipata asilimia 23.26 ya kura zote.

Wanajeshi hao wamezingira na kushikilia vituo vyote muhimu vya mawasiliano jana, siku moja kabla ya kuanza kwa kampeni za uchaguzi wa marudio zilizotarajiwa kuanza leo na kumalizika Aprili 21.

Wapinzani walionya kwamba hakuna sababu ya kufanya kampeni mapema jana, huku wakionya kwa yeyote atakayekaidi agizo hilo, lakini muda mfupi baadaye nchi hiyo ilitikiswa na taarifa za mapinduzi ya kijeshi.

Tangu kupata uhuru wake kwa nguvu za kijeshi mwaka 1974, jeshi na Serikali ya nchi hiyo vimekuwa katika nguvu inayoelekeana na muda mwingine mivutano, hivyo  kufanya nchi hiyo isiwe Rais aliyemaliza muda wake.

Milio ya risasi na mabomu ya kurushwa kwa mikono iliosikika katika mitaa mbalimbali kwenye mji mkuu wa nchi hiyo alfajiri ya kuamkia jana, huku ikizua hofu kubwa katika nchi hiyo ambayo iko katika kipindi cha kuelekea marudio ya uchaguzi mkuu.

“Tulishambuliwa kwa risasi na mabomu, tuloilazimika kujibu mapigo,” alisema mmoja wa maofisa wa polisi aliokuwa lindo katika makazi ya Gomes, akifafanua kuwa awali kiongozi huyo alikuwemo katika makazi hayo, lakini alifanikiwa kutoroka.

Moja ya vyanzo vya kijeshi kilikaririwa na AFP kikieleza kwamba wanamtafuta kwa juhudi zote Gomes bila kujali alikojificha na kwamba wana uhakika wa kumtia nguvuni.

Taarifa hizo zilieleza kwamba askari walitanda katika maeneo mengi ya mji uliogubikwa na giza usiku wa kuamkia jana, huku umeme ukiwa umekatwa na raia wakiwa wamejihifadhi majumbani mwao.

Awali, wanajeshi walishikilia jengo la makao makuu ya chama tawala cha nchi hiyo ambako vikosi zaidi ya 20 vimetapakaa katika eneo hilo na kuzuia matangazo ya redio na televisheni.

Vikosi hivyo pia vililizingira jingo la Ikulu ya Rais wan chi hiyo huku Rais anayemaliza muda wake akisimamia kipindi cha mpito, Raimundo Pereira akiwa hajulikani aliko.

Kumekuwa na mashaka ya kuibuka kwa vurugu katika uchaguzi wa marudio unaotarajiwa kufanyika kwenye taifa hilo masikini ambalo limekuwa likitawaliwa na vurugu za kisiasa, pia kujulikana kuwa miongoni mwa mataifa yanayopitisha madawa ya kulevya kati ya Amerika ya Kusini na Ulaya.

Upinzani nchini humo ukiongozwa na mgombea aliyeshika nafasi ya pili katika uchaguzi wa awali mwezi Machi mwaka huu, Kumba Yala, Rais wa zamani ambaye anadai kuwa mshindi katika awamu ya kwanza umetishia kugomea uchaguzi wa marudio Aprili 29 kwa madai kuwa kulikuwa na udanganyifu katika awamu ya kwanza.

Wagombea wakuu wa upinzani katika uchaguzi huo akiwemo Yala walisema jana kwamba hatua ya kugomea uchaguzi wa marudio itakuwa katika msingi wa kusimamia “haki”.
Uapinzani kwa pamoja ulipiga marufuku kushiriki katika kampeni zozote kuelekea uchaguzi wa marudio, huku Yala akionya kwamba “Yeyote atakayefanya kampeni atabeba jukumu la kile kitakachotokea”.

No comments:

Post a Comment