Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi CCM, Nape Nnauye akizungumza na waandishi wa habari Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, mtaa wa Lumumba, Dar es Salaam, kuhusu maamuzi ya kikao cha Kamati Kuu ya CCM iliyokutana  mjini Dar es Salaam, ambapo pamoja na mambo mengine imeridhia Rais Kikwete kuvunja Baraza la Mawaziri.
IFUATAYO NI TAARIFA ALIYOITOA KWA WAANDISHI WA HABARI.
Rais amepokea taarifa na maazimio ya Kamati ya wabunge wa CCM na Kamati ya uongozi ya wabunge wa CCM juu ya kilichotokea kwenye bunge lililopita mjini Dodoma.
      Taarifa hizo zimewasilishwa kwenye kamati kuu na kujadiliwa. Pamoja na taarifa hizo kamati Kuu imepokea taarifa ya jinsi Rais alivyojipanga kuchukua hatua za kuwawajibisha mawaziri na watendaji wa serikali na wale wa mashirika ya umma waliobainika kuhusika na ubadhirifu ulioinishwa na  taarifa ya Mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za Serikali, Kamati za kudumu za bunge na wabunge bungeni.
Kamati Kuu imeamua yafuatayo;
        1. Kamati Kuu inatambua na kuheshimu haki na wajibu wa wabunge kujadili utendaji wa serikali yao.Inapongeza juhudi za serikali kuhakikisha kuwa ripoti ya mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za serikali inajadiliwa kwa uwazi na hivyo kuibua mapungufu yaliyojadiliwa.
           2. Kamati Kuu imeridhika na imebariki uamuzi wa Rais   KULISUKA UPYA BARAZA LA MAWAZIRI na taasisi zingine zilizoanishwa katika ripoti hizo. Imesisitiza utekelezaji wa uamuzi huo ufanywe mapema iwezekanavyo.
           Aidha kamati Kuu imeipongeza Kamati Teule ya baraza la wawakilishi Zanzibar iliyoundwa kuchunguza utendaji katika sekta mbalimbali kwenye serikali ya mapinduzi Zanzibar kwa taarifa yao.
           Kamati Kuu inawapongeza wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa jinsi walivyojadili taarifa hiyo na pia Kamati Kuu inaipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kuipokea taarifa na kuanza kuifanyia kazi.